Breaking News

Gates Foundation yaipongeza Tanzania uboreshaji Afya ya msingi na kupunguza vifo vya Mama na Watoto




Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania imepongezwa kutokana na jitihada madhubuti za kuimarisha afya ya msingi na kupunguza idadi ya vifo vya kina mama wajawazito na watoto chini ya umri wa miaka mitano.

Hayo yameelezwa na Mkurugenzi Mkuu wa Gates Foundation Barani Afrika, Dkt. Paulin Basinga alipotembelea Hospitali ya Taifa Muhimbili (MNH) ambapo alipata fursa ya kuona jinsi inavyotoa mchango wake kwa Serikali kuimarisha upatikanaji huduma ngazi ya afya ya msingi, hospitali za rufaa za mikoa hadi Kanda na hatimaye kupunguza rufaa za wagonjwa kufika hospitalini hapo ikiwemo kupunguza rufaa za wagonjwa kwenda nje ya nchi.

Dkt. Basinga amesema taasisi anayoiongoza imefanya kazi na Serikali ya Tanzania katika maeneo ya uboreshaji programu za kilimo, masuala ya fedha kwa ujumla wake, sekta ya afya hususani kufanya tafiti zilizoibua afua mbalimbali za kupunguza vifo vya kina mama wajawazito na watoto chini ya umri wa miaka mitano.

Katika hatua nyingine, Dkt. Basinga ameipongeza MNH ambayo ni hospitali ngazi ya juu ya nne nchini kutokana na huduma za ubingwa na ubingwa bobezi inazotoa kwa wananchi wa ndani, mataifa jirani, mazingira bora ya utoaji huduma na utayari wa watoa huduma kuhudumia wananchi katika hospitali hiyo.

Kwa upande wake Mkurugenzi Mtendaji wa MNH, Prof. Mohamed Janabi amemshukuru Dkt. Basinga kutembelea hospitali hiyo na kumhakikishia kuwa hospitali hiyo kwa nafasi yake inafanya kazi kubwa kwa niaba ya Serikali katika kuimarisha huduma nchini ikiwemo huduma ngazi ya msingi hadi ngazi ya kanda




No comments