Breaking News

Kafulila: Watanzania anzisheni fursa za uwekezaji

   Mkurugenzi Mtendaji wa Ubia kati ya Sekta ya Umma na Sekta binafsi - (PPP) David Kafulila

.....awataka kutosubiri tangazo la zabuni za Serikali

....aeleza njia nne Sekta ya Umma, Binafsi zanavyofanya kazi pamoja

NA MWANDISHI WETU

Mkurugenzi Mtendaji wa Ubia kati ya Sekta ya Umma na Sekta binafsi - (PPP) David Kafulila amewashauri wafanyabiashara na wawekezaji nchini wasisubiri zabuni ya Serikali itangazwe ili waweze kupata fursa na badala yake wenyewe waanzishe fursa.

Ushauri huo Kafulila aliutoa jana katika mahojiano maalumu na chombo kimoja cha habari jijini Dar es Salaam akieleza namna Sekta ya Umma na Sekta Binafsi zinavyoweza kufanya kazi kwa pamoja.

Kamishna Kafulila alieleza kuwa Sheria ya Ubia kati ya Sekta ya Umma na Sekta Binafsi ina maeneo manne ambayo yanatoa nafasi kwa pande hizo mbili kuweza kufanya kazi kwa pamoja.

Alisema kuwa njia ya kwanza ni ile ambayo Serikali inahitaji kufanya mradi kwa utaratibu wa ubia, hivyo inauanda mradi husika kwa maana ya kufanya upembuzi yakinifu ambapo itaonesha sifa za mradi za kibiashara, kiuchumi na sifa nyingine.

Kwamba upembuzi huo ukishafanyika, mradi unapelekwa sokoni kwa maana ya kuutangaza ili kampuni binafsi zishindane na kuchukua fursa hiyo, ambapo alieleza kuwa njia hiyo Serikali inaanzisha yenyewe mradi na kuuweka sokoni.

“Njia ya pili ni ile ambayo Sekta Binafsi inaona fursa, kwa mfano inaweza kuwa jinsi ambavyo Serikali inaendesha Reli ya SGR labda kutoka Dar es Salaam mpaka Dodoma, mwekezaji anaweza kusema, ningepewa mimi kampuni binafsi ningeweza kufanya vizuri zaidi ya inavyofanya kwa faida yangu na kwa faida ya Serikali na kwa faida ya umma. Kwa hiyo hii ni ile ambayo Sekta Binafsi yenyewe imeichungulia fursa. Kimsingi fursa inakuwepo,” alitoa mfano Kamishna Kafulila na kuongeza,

“Na huu ni ujumbe kwa Watanzania ambao wapo katika masuara ya biashara na uwekezaji kwamba kwenye masuala ya ubia hauhitaji kusubiri zabuni ya Serikali itangazwe ili uweze kupata fursa na badala yake wewe mwenyewe unaweza kuanzisha fursa. Kimsingi fursa inakuwepo,”.

Alieleza kuwa ili kuanzisha fursa hiyo ni kupeleka kusudio la kuwekeza katika eneo kulani ambalo mamlaka ya Serikali inaendesha tofauti na maono yako kwa lengo la kuleta ufanisi au ubora zaidi katika mradi husika.

“Kimsingi unaleta sasa kusudio la kuwekeza katika hilo eneo ambalo wewe umeona kwamba mamlaka fulani ya Serikali inavyoendesha jambo fulani, mimi ningeweza kuendesha vizuri zaidi kwa faida yangu kibiashara, kwa faida ya Serikali kwa maana ya kutoa huduma. Hivyo sasa unaleta kusudio la kuwekeza kwenye kituo cha Ubia, ukishaleta kituo kinaita Mamlaka ya Serikali pamoja na wewe na kisha unawasilisha dhana yako hiyo ambayo unataka kuileta kwenye eneo husika. Basi mchakato kutokea pale ukiwekwa sawa sawa na kuonekana inafaa unapata fursa ya kuwekeza kwa utaratibu huo wa ubia ambao umetokana na wewe kuanzisha fursa,” aliongeza Kamishna Kafulila.

Hivyo alibainisha kuwa Sekta Binafsi inaweza kuangalia maeneo mbalimbali, ambayo inaweza kuwekeza kwa ubia ana Serikali ikiwemo Sekta za elimu, maji, miundombinu ya barabara, afya na maeneo kadha wa kadha ambayo Sekta binafsi inaona kuna fursa ya kibiashara kama ikisimamia na kuleta faida kibiashara kwa msalhi yake yenyewe pamoja na Serikali.

Kafulila alibainisha njia ya tatu kuwa ni ile ambayo Mamlaka ya Serikali inahitaji huduma kwa haraka, ufumbuzi wa jambo fulani kwa haraka huku taratibu za kibajeti na za kimanunuzi zitachukua muda mrefu, hivyo mamlaka ya Serikali inaweza kuzungumza moja kwa moja na mwekezaji mwenye uwezo na wakaingia mkataba kutekeleza mradi husika.

“Kwahiyo Mamlaka ya Serikali inaleta tu taarifa kwa Kituo cha Ubia, kwa mfano inasema tuna shida labda ya majosho ya kuogeshea ng’ombe na tunaona bajeti inachelewa kutekeleza jambo hili na tunahitaji pengine ndani ya miezi michache ijayo tuwe tunakamilisha hili jambo na mahitaji haya ni ya haraka. Kwahiyo hii ni sifa ya mradi ambao unaweza kukafanywa kwa mazungumzo ya moja kwa moja kwa sababu kuna muwekezaji ambaye anauwezo wa kufanya kazi hii,” alifafanua Kafulila na kueleza,

“Huo ni mfano tu, lakini kila eneo ambalo mamlaka ya Serikali ina uhitaji wa huduma fulani kwa haraka inaweza mamlaka hiyo kuomba kufanya majadiliano na mwekezaji mwenye uwezo moja kwa moja bila utaratibu huu ambao unatumika kwa maana ya ule utaratibu wa upembuzi,”.

Alisema njia ya nne ni ile ambayo inaitwa ‘special arrangement’, kwa maana ya makubaliano maalumu au utaratibu maalumu ambao unafayika kama kuna aina fulani ya uwekezaji ambao Serikali inauhitaji huku kukiwa na kampuni binafsi yenye uwezo wa kuufanya, lakini utekelezaji wake unakwamishwa na taratibu za kisheria.

“Kwahiyo aina hiyo ya uwekezaji ina ruhusu kampuni binafsi na Mamlaka ya Serikali kutengeneza makubaliano nje ya sheria inayosimamia ubia. Hata hivyo utaratibu huo hufanikiwa baada ya Tume ya Mipango kuridhia kwamba mradi huo ni wa kimakakati na una mazingira maalumu, lakini pia ni lazima Mwanasheria Mkuu wa Serikali ajiridhishe na zaidi Baraza la Mawaziri liridhie,” alieleza Kamishna Kafulila.

Hata hivyo Kafulila alisema kuwa utaratibu huo hufanyika kwa miradi mikubwa na yenye unyeti wake kiasi cha kukubaliana kufumua baadhi ya vifungu vya kisheria ili kuuruhusu mradi kutekelezwa.

Kafulila alieleza kuwa mfumo huu wa ubia ni kwa faida ya pande tatu, faida kwa mwekezaji kwa maana ya kwamba anapata biashara, faida kwa Serikali kwa maana ya kwamba inafanikisha upatikanaji wa mradi bila kutumia kodi, kukopa, kwahiyo inaipa fursa Serikali kufanikisha mradi husika bila presha ya kodi na mkopo, lakini pia ni faida kwa umma kwani huduma inapatikana kwa wakati bila kusubiri utaratibu wa Serikali kukopa na kutumia kodi.

Aliongeza kuwa, zaidi mradi wa ubia unaendeshwa na kampuni binafsi ambayo inatengeneza faida na kulipa kodi.

 

 

No comments