Breaking News

Vikundi vya kijamii vyashauriwa kujisajili kwenye mfumo wa wezesha Portal.

 Mkurugenzi Mtendaji wa Manispaa ya Morogoro, Bw. Emmanuel Mkongo akipokea nyenzo za ufundishaji wa elimu ya fedha kwa umma kutoka kwa Kamishina Msaidizi wa Idara ya Uendelezaj wa Sekta ya Fedha kutoka Wizara ya Fedha, Bi. Dionesia Mjema alipomtembelea ofisini kwake Mjini Morogoro

Vikundi vya Kijamii na huduma ndogo za fedha nchini vimetakiwa kujisajili katika mfumo wa wezesha portal ambao umeanza kutumika tangu mwezi Oktoba, 2023, ili kuweza kungiza taarifa za vikundi hivyo ikiwemo taarifa za biashara zao, namna wanavyokopa na kufanya marejesho ya mikopo yao.


Akizungumza katika mwendelezo wa program ya elimu ya fedha kwa umma iliyotolewa kwa wananchi wa Halashauri ya Manispaa ya Morogoro, Kamishina Msaidizi wa Idara ya Uendelezaji wa Sekta Ndogo ya Fedha kutoka Wizara ya Fedha, Bi. Dionesia Mjema, alisema ni muhimu watoa huduma ndogo za fedha wakajisajili na kupata leseni ya kutoa huduma hizo kwa wananchi kwa mujibu wa sheria za Benki Kuu ya Tanzania.
 
‘’Natoa wito kwa Taasisi za huduma ndogo za fedha ni muhimu wasajiliwe kwa mujibu wa Sheria ya Benki Kuu ya Tanzania, vilevile vikundi vyote vya huduma ndogo za fedha na vile vya kijamii ni lazima visajiliwe kwa mujibu wa Sheria ya Huduma Ndogo za Fedha ili viweze kunufaika na fursa mbalimbali za uwezeshaji kiuchumi zinazotolewa na Serikali’’. Alisema Bi. Mjema
 
Wananchi wa Halmashauri ya Morogoro Mjini wakifuatilia mada mbalimbali zilizotolewa na wataalam wa masuala ya fedha kutoka Wizara ya Fedha na Washirika wa sekta ya fedha nchini katika ukumbi wa Mbaraka Mwinshee Mjini Morogoro.

Bi. Mjema aliongeza kuwa ni vyema vikundi vya kijamii na huduma ndogo za fedha vikaharakisha kujisajili kwenye mfumo wa Wezesha Portal kwa kufanya hivyo kutawasaidia kuunganishwa na fursa mbalimbali zilizopo kwenye mifuko na program za uwezeshaji wananchi kiuchumi pamoja na Taasisi za fedha zinazotoa mikopo kwa riba nafuu inayotolewa kwa vijana wajasiriamali na makundi maalum.
 
Awali, akizungumza na ujumbe wa Halamshauri ya Manispaa ya Morogoro ukiongozwa na Mkurugenzi Mtendaji wa Manispaa ya Morogoro, Bw. Emmanuel Mkongo, Bi. Mjema alisema kuwa lengo la Serikali ni kuvihudumia vikundi vyote vya kijamii kulingana na shughuli wanazofanya ili iwe rahisi kuwajengea uwezo kupitia program mbalimbali zinaotolewa na serikali kupitia Wizara ya Fedha na wanavikundi hao waweze kukuza biashara zao.
 Afisa Usimamizi wa Fedha kutoka Wizara ya Fedha, Bw. Stanley Kibakaya akizungumza na wananchi waliohudhuria program maalum ya elimu ya fedha iliyotolewa kwa wananchi hao katika ukumbi wa Mbaraka Mwinshee Mjini Morogoro.

‘’Vikundi vya huduma ndogo na vile vya kijamii tunataka vikae kwa cluster, mfano vikundi vya mafundi cherehani, saluni, mafundi seremala na vingine, kwa sababu ni rahisi kwenye hizi program zetu kuja kuwajengea uwezo ambao utawasaidia kukuza biashara zao’’. Aliongeza Bi. Mjema
 
Aidha alisema kuwa ni vyema Wakurugenzi wa Halmashauri wakatenga maeneo maalum kwa vikundi hivyo kwa ajili ya kufanya shughuli zao ili iwe rahisi kwa serikali kuwapelekea fursa hizo za kuwawezesha kiuchumi kwa kuwa vitakuwa vinafanya shuhuli zao katika maeneo yaliyo rasmi.
 
Program ya elimu ya fedha kwa umma inatolewa ili kuwajengea wananchi uelewa wa masuala yote ya fedha yakiwemo ya uwekezaji na mikopo ili kupunguza athari wanazozipata wananchi kutokana na wimbi kubwa lililojitokeza sasa la huduma ya mikopo isiyo rasmi maarufu kama mikopo ya kausha damu.


Kamishina Msaidizi wa Idara ya Uendelezaj wa Sekta ya Fedha, Bi. Dionesia Mjema akitoa mada kuhusu masuala ya fedha na umhimu wa kusajili vikundi vya kutoa huduma ndogo za fedha na vile vya kijamii kwa wananchi wa Manispaa ya Morogoro (hawapo pichani) kwenye program maalum ya elimu ya fedha iliyotolewa kwa wananchi hao katika ukumbi wa Mbaraka Mwinshee Mjini Morogoro.

No comments