Breaking News

TANESCO KUOKOA BILIONI 30 KILA MWAKA MKOA WA KAGERA UTAKAPOINGIA KWENYE GRIDI YA TAIFA


Na Charles Kombe, Dar es Salaam

Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO) litaokoa kiasi cha Shilingi bilioni 30 kila mwaka baada ya Ujenzi wa njia  ya kusafirisha umeme  ya  Benaco-Kyaka kukamilika jambo litakaloimarisha hali ya upatikanaji wa umeme katika Mkoa wa Kagera kwa kuwezesha  Wilaya za Kyerwa, Karagwe, Misenyi, Muleba, Bukoba vijijini na Manispaa ya Bukoba  kuunganishwa katika Gridi ya taifa. 

Hayo yamebainishwa na Mkurugenzi Mtendaji wa TANESCO Mha. Gissima Nyamo – Hanga wakati wa hafla ya utiaji saini wa mkataba na Mhandisi Mshauri  (Shaker Consultancy  Group) kutoka nchini  Misri ikishirikiana  na   Kampuni ya usimamizi  miradi  ya umeme ya Saudi  Arabia (PDC)  leo Juni 12, 2024 katika ukumbi wa mikutano wa Shirika Masaki, Dar es salaam kwa ajili ya kuandaa nyaraka za manunuzi ya wakandarasi wa ujenzi pamoja na usimamizi wa ujenzi  wa   njia  ya kusafirisha umeme ya msongo wa Kilovoti  (220) ya Benaco hadi Kyaka Mkoani Kagera.

“Kwa sasa matumizi kwa mwezi ya kununua umeme kutoka Uganda unaotumika mkoa wa Kagera ni karibu shilingi bilioni 2.6 ambayo ni karibu bilioni 30 kwa mwaka.  Pindi mkoa wa Kagera utakapounganishwa kwenye gridi ya taifa, kiwango hicho cha fedha kitaokolewa na kuwezesha fedha hiyo  kutumika kuboresha miundombinu yetu ya umeme katika maeneo mengine”, amesema Mha. Nyamo – Hanga

Ameongeza kuwa, ujenzi wa njia hiyo ya kusafirisha umeme  ya  Benaco-Kyaka utaimarisha hali ya upatikanaji wa umeme katika Mkoa wa Kagera ambapo  Wilaya za Kyerwa, Karagwe, Misenyi, Muleba, Bukoba vijijini na Manispaa ya Bukoba  zitaunganishwa katika Gridi ya taifa ambazo zimekuwa zikipokea umeme kiasi cha Megawati 21 kutoka  nchini Uganda kupitia kampuni ya kusafirisha umeme ya (UETCL).

Kwa upande wake Mkurugenzi Mtendaji wa Shaker Consultancy  Group Dr. Ismail Shaker amesema kuwa kwa zaidi ya miaka nane wamekuwa wakifanya kazi na nchi za Afrika na Tanzania ni nchi ya kipekee wanayopenda kushirikiana nayo katika sekta ya umeme.

“Napenda kuishukuru TANESCO pamoja na Mkurugenzi mtendaji kwa kutuamini na nichukue nafasi hii kumhakikishia na kuwahakikishia wote hapa ya kuwa tutafanya kila tunaloweza kufikia matarajio. Tunafahamu TANESCO inataka kuifanya nchi hii kuwa kinara kwenye uzalishaji wa umeme na tunafuraha kuwa sehemu ya timu hii”, amesema Dr. Shaker

Ujenzi wa mradi  huu  utagharimu kiasi cha Dola za kimarekani Milioni 135. 4 ukihusisha ujenzi wa njia ya kusafirisha Umeme  ya umbali wa kilometa 166.17 kutoka Benaco mpaka Kyaka,ujenzi wa kituo kipya cha kupoza umeme cha Benaco na kukiongezea uwezo wa kituo cha kupoza umeme Kyaka kilichopo sasa.

Mradi huu utagharamiwa na Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kiasi cha Shilingi za kitanzania  Bilioni 6.2 wadau wa maendeleo kutoka Mfuko wa Maendeleo wa Saudi (SFD) Dola za Marekani Milioni 13,Mfuko wa Maendeleo wa Abudhabi Dola za Marekani Milioni 30 na Mfuko wa Maendeleo ya Kimataifa wa OPEC ambao utachangia kiasi cha  Dola milioni 60 za Marekani.

Mkandarasi wa ujenzi wa mradi huu anatarajiwa kupatikana  mwezi Disemba 2024 na utekelezaji wa mradi utakamilika Disemba 2026.


No comments